Yanga imetuma salamu kwa watani zao Simba ambao wanakutana nao katika mchezo unaofuata wakiichapa JKT Tanzania mabao 5-0 katika mchezo wa ligi kuu ya NBC uliopigwa uwanja wa KMC Complex.
Mohamed Hussein 'Zimbwe Jr' ndiye aliyefunga bao la mapema kipindi cha kwanza akimalizia pasi ya Prince Dube ambaye awali kulikuwa na taarifa angekosa mchezo wa leo lakini amerejea kwa wakati.
JKT Tanzania walihimili mikiki mikiki ya Yanga kwenye kipindi cha kwanza kwani mpaka mapumziko walikuwa wamefungwa bao moja tu.
Hata hivyo vijana wa kocha Pedro Goncalves walirejea kipindi cha pili wakiwa moto zaidi wakifanikiwa kuongeza mabao manne.
Laurindo Aurelio 'Depu' ameendeleza kasi yake ya kuweka mipira kimiani akifunga bao la pili baada ya krosi ya Israel Mwenda huku Mudathir Yahya akiongeza bao la tatu dakika mbili baadae akimalizia mpira uliogongwa mwamba.
Dube ambaye alichaguliwa nyota wa mchezo akaweka kambani bao la nne akimalizia krosi ya Buba Jammeh huku Shakhan Khamis akipigilia msumari wa tano dakika za lala salama.
Wachezaji wa Yanga leo ni kama walisikia maoni ya mashabiki wao baada ya kutocheza vyema mchezo uliopita. Walikuwa hatari kila waliposhambulia lango la JKT Tanzania.
Ni ushindi ambao umeirudisha rasmi Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi wakiishusha JKT Tanzania hadi nafasi ya piili.



