Homa ya pambano la watani wa jadi ligi kuu ya NBC kati ya Yanga dhidi ya Simba inazidi kupanda zikisalia takribani siku nne tu mchezo huo kupigwa visiwani Zanzibar.
Mchezo huo namba 54 utapigwa uwanja wa New Amaan Complex siku ya Jumapili, March 1 saa 3 usiku.
Klabu ya Yanga imeondoka mapema leo jijini Dar es salaam kuelekea Zanzibar kukamilisha maandalizi yake huku watani zao Simba wakitarajiwa kurejea jijini Dar es salaam leo wakitokea Dodoma ambako jana walilazimishwa suluhu ya bila kufungana dhidi ya Dodoma Jiji katika mchezo wa ligi kuu ya NBC.
Kocha Mkuu wa Simba Steve Barker amesema kikosi chake kitaelekea Zanzibar mapema ili kupata muda wa kukamilisha maandalizi kuelekea mtanange huo.
Simba inaweza kuwa kwenye presha kubwa ya matokeo pengine kuliko Yanga kufuatia matokeo ya sare waliyopata jana.
Yanga iko kileleni mwa msimamo wa ligi ikiwa na alama 28 baada ya mechi 10 huku Simba ikishika nafasi ya tatu ikiwa na alama 23 baada ya mechi 10.
Tayari Yanga inaizidi Simba alama 5 hivyo kama watapoteza mchezo huo Jumapili watakuwa nyuma ya Yanga kwa alama nane ambapo watajiweka katika mazingira magumu kwenye mbio za ubingwa.
Lakini pia Yanga imeshinda mechi nne mfululizo zilizopita kwenye ligi, Wananchi watakuwa wakisaka rekodi nyngine ya kuendeleza ubabe dhidi ya watani zao hao