Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Wallace Karia amesema mwamuzi yoyote atakayeharibu mchezo wa kesho wa dabi ya Kariakoo kati ya Yanga na Simba, watamfungia maisha kujihusisha na mpira wa miguu.
Akizungumza kwenye Mkutano Mkuu wa 20 wa TFF unaofanyika Kahama mkoani Shinyanga mapema leo, Karia alisema mbali na kumfungia maisha pia watamfungulia mashataka.
“Naomba niseme hapa kwenye Mkutano Mkuu na waamuzi wanisikie, atakayeharibu mchezo wa kesho hatutamuacha salama, malalamiko yamekuwa mengi na yanaharibu taswira ya mchezo,” alisema Karia.
Jana Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) lilimtangaza Nassor Mwinchui mwamuzi kutoka Tanga ndiye mwamuzi wa kati mchezo kati ya Yanga dhidi ya Simba utakaopigwa kesho Jumapili, March 1 katika uwanja wa New Amaan Complex.
Mwamuzi Msaidizi I ni Kassim Mpanga kutoka Dar es salaam wakati Msaidizi II ni Hamdan Said kutoka Mtwara,
Ramadhan Kayoko ni mwamuzi wa akiba na Israel Mjui akiwa mtathmini waamuzi.



