Mchezo wa ligi kuu ya NBC kati ya Yanga dhidi ya Simba uliopigwa uwanja wa New Amaan Complex, umemalizika kwa matokeo ya suluhu ya bila kufungana.
Unaweza kusema timu bora leo Simba imenyimwa alama tatu kwani Suleiman Mwalimu alifunga bao halali ambalo lilikataliwa kimakosa na mwamuzi msaidizi Kasim Mpanga.
Simba iliuanza mchezo huo kwa kasi na pengine Inno Loemba na Annicet Oura wangeweza kufunga bao mapema kama sio uimara wa golikipa wa Yanga Djigui Diarra.
Dakika zote 45 za kipindi cha kwanza ni Simba iliyokuwa bora uwanjani kilichokosekana ni mabao tu.
Kipindi cha pili mwanzoni Yanga ilikuwa bora lakini kuanzia dakika ya 60 ni Simba iliyorejesha umiliki wa mechi na Mwalimu aliyeingia kipindi cha pili alifunga bao lililokataliwa kwa offside.
Elie Mpanzu nae aliyeingia dakika ya 75 kipindi cha pili alikosa nafasi wakati mchezo huo ukielekea ukingoni.
Ni kiwango bora kwa Simba katika mchezo huo, pengine hii ni dalili njema kwa Simba kwenye mbio za ubingwa.
Matokeo hayo yanaendelea kuiweka Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi ikifikisha alama 29 huku Simba ikiendelea kusalia nafasi ya tatu ikiwa na alama 24.



