Mchezo wa ligi kuu ya NBC kati ya Azam Fc dhidi ya Yanga ulipangwa kuchezwa March 15, umehamishiwa uwanja wa Azam Complex baada ya uwanja wa Benjamin Mkapa kufungwa kwa ajili ya ukarabati.
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Azam FC, Thabit Zakaria ‘Zaka Zakazi’ amethibitisha kuwa mchezo huo wa kwanza dhidi ya Yanga katika ligi utachezwa Uwanja wa Azam Complex.
“Mechi hiyo itachezwa hapa uwanja wa nyumbani na siyo kwa Mkapa kama ilivyozoeleka, hivyo tunawakaribisha sana mashabiki waje kushuhudia mechi kubwa na nzuri,” alisema Zaka Zakazi.
Msimu uliopita mechi zote mbili za Ligi Kuu Bara zilizokutanisha timu hizo zilipigwa uwanjani hapo. Mechi ya duru kwanza Azam Fc iliibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Gibril Sillah, kisha duru la pili Yanga ikashinda 2-1. Mabao ya Yanga yalifungwa na Pacome Zouzoua na Prince Dube wakati Azam mfungaji alikuwa Lusajo Mwaikenda.
Kwa sasa Azam inashika nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 23, wakati Yanga ikiongoza na pointi 29, zote zimecheza mechi 11.
Kabla ya dabi hiyo, zote zitashuka dimbani mara tatu, zikiwamo mechi mbili za ligi na moja Kombe la Shirikisho (FA).
Machi 5, Yanga itacheza dhidi ya Singida Black Stars wakati Azam ikipambana na Tanzania Prisons, katika mechi za Ligi Kuu Bara zote zikiwa ugenini.
Machi 8, zote zitakuwa nyumbani katika hatua ya 32 Bora ya Kombe la Shirikisho (FA), Yanga ikicheza dhidi ya Polisi Tanzania na Azam dhidi ya Mbeya Kwanza.
Machi 11, Azam itakuwa ugenini kucheza dhidi ya Dodoma Jiji, kisha Machi 12, Yanga pia itakuwa ugenini kucheza dhidi ya Tanzania Prisons.



