Michuano ya UEFA Champions League iliendelea Jumanne usiku, Machi 10, 2026 kwa mechi za hatua ya 16 bora (Round of 16 – mkondo wa kwanza) huku baadhi ya timu zikianza kujijengea nafasi nzuri ya kusonga mbele robo fainali. Mechi hizo zilishuhudia ushindi mkubwa, mshangao na sare ya dakika za mwisho.
Atlético Madrid 5–2 Tottenham Hotspur
Klabu ya Atlético Madrid ilipata ushindi mkubwa wa mabao 5–2 dhidi yaTottenham Hotspur katika uwanja wa Metropolitano. Ushindi huo umeiweka Atlético kwenye nafasi nzuri ya kufuzu robo fainali kabla ya mchezo wa marudiano nchini England.
Timu hiyo ya Hispania ilionyesha ubora mkubwa katika safu ya ushambuliaji huku ikitawala sehemu kubwa ya mchezo na kuwapa wakati mgumu wageni wao. Matokeo hayo yanamaanisha Tottenham italazimika kufanya kazi kubwa katika mechi ya pili ili kugeuza matokeo hayo.
Atalanta 1–6 Bayern Munich
Bayern Munich walitoa onyesho kali baada ya kuichapa Atalanta kwa mabao 6–1 katika mchezo uliochezwa Italia.
Ushindi huo mkubwa umeifanya Bayern kuwa karibu sana kufuzu hatua ya robo fainali, kwani Atalanta sasa wanahitaji ushindi mkubwa sana katika mechi ya marudiano nchini Ujerumani.
Klabu ya Galatasaray ya Uturuki ilipata ushindi mwembamba wa 1–0 dhidi ya Liverpool katika mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa RAMS Park mjini Istanbul.
Bao pekee la mchezo lilifungwa mapema dakika ya 7 na Mario Lemina kwa kichwa baada ya mpira wa kona uliopigwa na wachezaji wenzake. Ushindi huo umeipa Galatasaray faida ndogo kabla ya safari ya kwenda Anfield kwa mechi ya marudiano.
Newcastle United 1–1 Barcelona
Katika mchezo mwingine, Barcelona walinusurika kupoteza baada ya kutoka sare ya 1–1 dhidi ya Newcastle United katika uwanja wa St James’ Park.
Newcastle walitangulia kufunga, lakini Barcelona walipata bao la kusawazisha katika dakika za mwisho kupitia penalti ya Lamine Yamal, jambo lililowapa matumaini makubwa kabla ya mechi ya marudiano nchini Hispania.



