Kocha Mkuu wa Simba Steve Barker amesema amekiandaa kikosi chake kikamilifu kuelekea mchezo wa ligi kuu dhidi ya TRA United utakaopigwa kesho Jumamosi, March 14 katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid mkoani Arusha.
Akizungumza katika mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Barker amesema ligi ni ngumu na wanapaswa kucheza katika kiwango bora kwenye kila mchezo.
Kocha huyo wa zamani wa Stellenbosch ya Afrika Kusini, amesema nyota wake wote wako tayari kwa mchezo huo na dhamira yao ni kuondoka na alama zote tatu kama walivyofanya kwenye mchezo uliopita dhidi ya Singida BS.
"Sisi tumejiandaa vyema kwa ajili ya mchezo, nafahamu hautakuwa mchezo mwepesi. Kila mechi ni ngumu na tunapaswa kucheza katika ubora wetu kupata mtokeo mazuri."
"Ni lazima tucheze kwa kuzingatia mpango tulioandaa kwa ajili ya mchezo huu, nafahamu kama hatutafanya hivyo mchezo unaweza kuwa mgumu."
"Tumekuwa na maandalizi ya kimbinu kwa zaidi ya miezi miwili sasa, maandalizi yetu hayazingatii mchezo mmoja bali tunajiandaa kimfumo na kuhakikisha tunatimiza mipango yetu katika kila mechi. Tunataka kumiliki mchezo na kuwapa wapinzani wetu wakati mgumu katika muda wote wa mchezo," alisema Barker.
Simba ilitua Arusha jana ambao leo inatarajiwa kukamilisha maandalizi yake ya mwisho katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid ambapo mchezo huo utapigwa.



