Goncalves, Ibenge wafunguka maandalizi ya Dar Derby

Joel JJ By Joel JJ • 14th March 2026


Goncalves, Ibenge wafunguka maandalizi ya Dar Derby

Kocha Mkuu wa Yanga Pedro Goncalves amesema kikosi chake kiko tayari kwa mchezo wa ligi kuu dhidi ya Azam Fc ambao utapigwa kesho Jumapili katika uwanja wa Benjamin Mkapa.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari mapema leo, Goncalves amesema mchezo dhidi ya Azam Fc utakuwa mgumu kwa sababu wanakutana na timu ngumu.

Goncalves amesisitiza kuwa wachezaji wake watakwenda kupambana kwenye mchezo huo dhamira yao ikiwa kuibuka na ushindi.

"Tunakwenda kukabili miongoni mwa timu ngumu kwenye ligi, Azam Fc wamekuwa na kiwango kizuri hata kwenye michuano ya kombe la Shirikisho (CAFCC)."

"Lakini pia tulicheza nao fainali ya kombe la Mapinduzi Zanzibar, ni timu ngumu inayofundishwa na kocha mwenye uzoefu mkubwa na soka la Afrika."

"Kwangu mimi ni jambo zuri kucheza uwanja wa Benjamin Mkapa, hii itakuwa mara ya kwanza kucheza katika uwanja huu tangu nifike hapa."

"Tumekuwa na ratiba ngumu, tumepata siku mbili tu za kujiandaa na mchezo huu, jana haikuwa rahisi kwetu, tulikuwa na program ya 'recovery' na leo ndio tutakamilisha maandalizi kuelekea mchezo huo."

"Lakini tuko imara, vijana wangu wanaelewa kile wanapaswa kufanya licha ya kuwa tumekuwa tukicheza katika viwanja vyenye hali tofauti."

"Hivyo utakuwa mchezo mgumu kwa sababu tunakutana na timu ngumu lakini naamini wachezaji wangu wako tayari wakiwa na ari, na morali kubwa ya kushinda mchezo huo," alisema Goncalves.  

Nae mkufunzi wa Azam Fc Florent Ibenge amesema anatambua hautakuwa mchezo mwepesi kwani wanakwenda kucheza dhidi ya timu bora zaidi nchini katika misimu minne 

Hata hivyo Ibenge ameonyesha hakufurahishwa mchezo huo kupelekwa uwanja wa Benjamin Mkapa akiamini mchezo huo ulipaswa kupigwa uwanja wa Azam Complex.

"Mchezo huu nafikiri ulipaswa kuchezwa Azam Complex, ndio uwanja wetu wa nyumbani. Kucheza uwanja wa Mkapa inawapa faida Yanga kwani ni kama uwanja wao wa nyumbani na tutacheza mechi mbili dhidi yao hapa"

"Tunatambua tunakwenda kucheza na timu bora zaidi kwa sasa hapa Tanzania, Azam Fc tunapambana kupunguza gap lililopo kati yetu na wao," alisema Ibenge.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.