Como ni hadithi ya kusisimua Serie A

Joel JJ By Joel JJ • 16th March 2026


Como ni hadithi ya kusisimua Serie A

Klabu ya Como inaendelea kuwa moja ya hadithi kubwa za mafanikio katika Serie A msimu wa 2025/26, chini ya uongozi wa kocha wao, Cesc Fabregas. Siku ya Jumapili, Machi 15, 2026, Como ilipata ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya AS Roma, ushindi uliowasukuma hadi nafasi za juu kwenye msimamo wa Serie A.

Roma ndio waliokuwa wa kwanza kupata bao mapema katika mchezo huo kupitia Donyell Malen, aliyefunga kwa mkwaju wa penalti baada ya Stephan El Shaarawy kuangushwa ndani ya eneo la hatari. Hata hivyo, Como walirejea kwa nguvu kipindi cha pili kufuatia mabadiliko ya kimkakati ya kocha Fabregas.

Mshambuliaji Tasos Douvikas aliisawazishia Como kabla ya beki Diego Carlos kufunga bao la ushindi, na kuwapa wenyeji alama tatu muhimu katika mbio za kufuzu michuano ya Ulaya. Ushindi huo uliiwezesha Como kupanda hadi nafasi ya nne kwenye msimamo wa Serie A. 

Mafanikio ya Como chini ya Fabregas

Tangu kuchukua jukumu la kocha mkuu, Fabregas ameigeuza Como kuwa timu inayoshindana na vigogo wa Serie A. Klabu hiyo ilipanda daraja mwaka 2024 na sasa imejipambanua kama moja ya timu zinazoweza kushindana kwa nafasi za Ligi ya Mabingwa Ulaya. 

Mbali na kufanya vizuri katika ligi, Como pia imefika hatua ya nusu fainali ya Coppa Italia, mafanikio makubwa kwa klabu ambayo kwa muda mrefu haikuwa ikionekana kwenye ushindani wa juu nchini Italia. 

Fabregas alivyokosoa tukio la baada ya mechi

Baada ya ushindi huo, Fabregas pia aliongea wazi kuhusu tukio la baada ya mchezo lililomhusisha kocha wa Roma, Gian Piero Gasperini. Fabregas alieleza kutoridhishwa kwake baada ya kocha huyo kudaiwa kukataa kumpa mkono wa pongezi baada ya mechi, akisisitiza umuhimu wa heshima katika soka.

Kauli hiyo iliongeza mjadala mkubwa katika vyombo vya habari vya michezo nchini Italia, huku baadhi ya wachambuzi wakisema ushindi wa Como umeonyesha jinsi timu hiyo inavyoendelea kukua chini ya kocha huyo aliyewahi kutanba na klabu za Barcelona na Arsenal.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.