Mchezo wa ligi kuu ya NBC kati ya TRA United dhidi ya Yanga uliopigwa uwanja wa Sheikh Amri Abeid mkoani Arusha umemalizika kwa matokeo ya suluhu ya bila kufungana.
Ni mchezo ambao haukuwa na mashambulizi mengi, wenyeji TRA United wakikaa nyuma kuzuia wakitumia mashambulizi ya kushitukiza huku Yanga licha ya kutawala mchezo kwa muda mwingi, walikosa kasi katika kutengeneza mashambulizi yao.
TRA United walimaliza wakiwa 10 baada ya Mzamiru Yassin kutolewa nje dakika ya 75 akionyeshwa kadi ya pili ya njano baada ya kumfanyia madhambi Mohamed Hussein.
Dakika za lala salama TRA United walifanya shambulizi kubwa ambalo Yanga watamshukuru mlinda lango Djigui Diarra aliyewaweka salama na kuondoka na alama moja
Ni sare ya pili mfululizo Yanga wanapata huku ikiwa ni sare ya nne msimu huu. Bado Yanga inaendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa ligi ikifikisha alama 37.



