Simba, Pamba Jiji, Azam Fc, Mashujaa viwanjani leo

Joel JJ By Joel JJ β€’ 19th March 2026


Simba, Pamba Jiji, Azam Fc, Mashujaa viwanjani leo

Ligi Kuu ya NBC inaendelea leo ambapo mechi mbili zinatarajiwa kupigwa mkoani Mwanza na kule Kigoma mwisho wa reli.

Jijini Mwanza Simba Sc itakuwa ugenini kuikabili Pamba Jiji kwenye mchezo utakaopigwa saa 10 jioni.

Ni wazi utakuwa mchezo mgumu unaozikutanisha timu mbili ambazo kwenye mechi zilizopita kati yao, nyasi ziliumia.

Pamba Jiji imeufanya uwanja wa CCM Kirumba kuwa mgumu kwa wapinzani msimu huu, wakulima hao wa Pamba wakishika nafasi ya 6 kwenye msimamo wa ligi.

Hata hivyo wanakutana na Simba ambayo kwa sasa imeimarika zaidi ikionyesha dhamira ya kurejesha taji la ligi kuu Msimbazi baada ya kulikosa kwa misimu minne iliyopita.

Simba ilitua jijini Mwanza juzi usiku, jana vijana wa kocha Steve Barker wakafanya mazoezi yao ya mwisho katika dimba la CCM Kirumba.

Baada ya watani zao Yanga kudondosha alama katika mechi mbili zilizopita, hii ni nafasi kwa Simba kupunguza gap la pointi baina ya timu hizo.

Kimahesabu kama Simba itashinda mechi zake zote za viporo, gap la pointi kati yake ya Yanga itasalia alama moja tu hatua ambayo itaweka wazi zaidi mbio za ubingwa wa ligi msimu huu.

Mchezo mwingine utapigwa Kigoma ambapo Mashujaa Fc wataialika Azam Fc kutoka jijini Dar es salam.

Hii ni mechi nyingine ngumu inayotarajiwa kuwa na upinzani mkali. Tangu ujio wa kocha Jamhuri Kiwhelo 'Julio' kwenye kikosi cha Mashujaa Fc, kuna upepo umebadilika.

Azam Fc watahitaji kufanya kazi ya ziada kuondoka na alama zote tatu mbele ya Mashujaa.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.