Mwenendo usioridhisha wamuweka matatani kocha Yanga

Joel JJ By Joel JJ β€’ 23rd March 2026


Mwenendo usioridhisha wamuweka matatani kocha Yanga

Wakati tetesi zikiendelea kushika kasi juu ya hatma ya kocha mkuu wa Yanga Pedro Goncalves, ni wazi wananchi wanahitaji kutumia vyema kipindi hiki cha mapumziko ya FIFA kujiimarisha ili warejee wakiwa imara zaidi.

Licha ya kuendelea kuwa kileleni mwa msimamo wa ligi, mwenendo wa mabingwa hao watetezi katika mechi za karibuni umewapa mashaka mashabiki ambao wanaamini kama hakutakuwa na mabadiliko huenda msimu huu wakawa na kazi ngumu ya kutetea ubingwa wao.

Ukiacha changamoto ya mejeruhi na ratiba ngumu, malalamiko yalianza mapema tangu wakati Yanga inashiriki michuano ya ligi ya mabingwa, ikikomea hatua ya makundi baada ya kumaliza nafasi ya tatu kundi B.

Mpaka sasa baada ya kucheza mechi 16 za ligi, Yanga iko nyuma ya kile walichofanya msimu uliopita. Wamekusanya alama 38 alama 4 pungufu ya zile walizokusanya msimu uliopita katika nyakati kama hizi

Msimu uliopita Yanga ilitwaa taji la ligi kuu na pointi 82 baada ya kucheza jumla ya mechi 30, ikishinda 27, sare moja na kupoteza mbili, huku ikifunga mabao 83 yakiwa mengi zaidi kuliko timu nyingine na kuruhusu kumi, ambayo ni machache zaidi.

Hata hivyo mpaka sasa Yanga imedondosha alama 10 katika mechi 16, wakati msimu uliopita walidondosha alama nane tu katika mechi 30.

Yanga imetoka sare tano dhidi ya Mbeya City, Simba, TRA Unted, Azam na Mtibwa Sugar na hivyo kudondosha idadi hiyo ya pointi wakati msimu uliopita timu hiyo ilitoka sare mchezo mmoja pekee dhidi ya JKT Tanzania na ikapoteza michezo miwili dhidi ya Azam na Tabora United (TRA).

Mabosi wa Yanga wanatarajiwa kukutana kujadili mwenendo huo wa timu na haitashangaza yakifanyika mabadiliko kwenye benchi la ufundi.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.