Shirikisho la Ligi ya Ufaransa (LFP) limeamua kuahirisha mchezo wa ligi kati ya RC Lens na Paris Saint-Germain, licha ya upinzani uliowekwa na Lens hapo awali.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka RMC Sport, uamuzi huo umefanywa ili kuipa PSG muda wa kutosha kujiandaa na mchezo wao muhimu dhidi ya Liverpool katika michuano ya UEFA Champions League.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa, kufuatia kuahirishwa kwa mechi hiyo, PSG sasa itakuwa na mapumziko ya wiki nzima kabla ya kuvaana na Liverpool katika mchezo wa robo fainali, hali inayoweza kuwapa faida kubwa ya kimwili na kiufundi.
Hata hivyo, hali ni tofauti kwa upande wa Liverpool, ambao wanakabiliwa na ratiba ngumu zaidi. Timu hiyo itacheza dhidi ya Manchester City siku nne kabla ya mchezo wa kwanza dhidi ya PSG, na kisha kukutana na Fulham FC siku tatu kabla ya mchezo wa marudiano.
Mabadiliko haya ya ratiba yameibua mjadala mkubwa kuhusu usawa wa ushindani, huku baadhi wakiona kuwa PSG wamepata faida muhimu kuelekea pambano lao na Liverpool katika hatua za mtoano.



