Tiketi zote zimeuzwa kwa ajili ya mchezo wa kirafiki kati ya Senegal na Peru , utakaochezwa Jumamosi hii katika dimba la Stade de France.
Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua takribani mashabiki 80,000 unatarajiwa kujaa, kufuatia mahitaji makubwa ya tiketi yaliyozidi matarajio.
Mchezo huo unatajwa kuwa wa kipekee, ukiwa pia sehemu ya shamrashamra za kusherehekea ushindi wa Africa Cup of Nations 2025 ambao Senegal wanadai kuutwaa.
Ripoti zinaeleza kuwa kabla ya kuanza kwa mchezo huo, kutakuwa na hafla maalum ya kuonyesha kombe hilo kwa mashabiki, hatua inayokuja wakati kukiwa na mvutano kufuatia maamuzi ya Confederation of African Football (CAF) kuhusu hatima ya ubingwa huo.
Licha ya mabishano hayo, mashabiki wa Senegal wameendelea kuonyesha mshikamano mkubwa kwa timu yao, hali iliyochangia kuuzwa kwa tiketi zote mapema.
Waandalizi wa mechi hiyo wamesema kuwa maandalizi yote yamekamilika na usalama umeimarishwa ili kuhakikisha tukio hilo linafanyika kwa mafanikio.
Mchezo huo unatarajiwa kuwa kivutio kikubwa kwa mashabiki wa soka, ukiwa na mchanganyiko wa ushindani wa kirafiki pamoja na sherehe za mafanikio ya timu ya Senegal.



