Ramovic aingia kwenye mgogoro na CR Belouizdad

Joel JJ By Joel JJ β€’ 29th March 2026


Ramovic aingia kwenye mgogoro na CR Belouizdad

Kocha raia wa Ujerumani, Sead Ramovi, amesimamishwa kwa muda na klabu ya CR Belouizdad baada ya mvutano mkali kati yake na uongozi wa klabu hiyo. Hatma yake sasa inasubiri uamuzi wa kamati ya nidhamu ya klabu utakaotolewa Jumanne ijayo.


Kisa kilichozusha mgogoro

Taarifa zinaeleza kuwa rais wa klabu, Badreddine Bahloul alimwalika Ramovic kuhudhuria kikao cha dharura majira ya saa 4 usiku, huku akielekezwa kufika peke yake. Ramovic, hata hivyo, alikataa wito huo akidai hakupokea taarifa yoyote rasmi, hakupokea barua, barua pepe wala mawasiliano mengine ya kiofisi. Aliomba kikao kifanyike kwa utaratibu rasmi na ndani ya saa za kazi.

Mvutano ulizidi pale rais wa klabu alipotaka kuingilia chumba cha kubadilishia nguo wakati Ramovic akiwa katika kikao na wachezaji, akipitia mchezo uliopita na kuandaa mechi inayofuata.

Kocha huyo alisisitiza nidhamu na umakini wa timu, akiwataka viongozi kusubiri hadi kikao hicho kitakapomalizika kabla ya kuingilia shughuli za benchi la ufundi. Uongozi wa klabu uliripotiwa kutoridhishwa na msimamo huo.


Hatua za kisheria

Baada ya matukio hayo, CR Belouizdad ilichukua uamuzi wa kumsimamisha Ramovic kwa muda, ikisubiri uchunguzi wa ndani na maamuzi zaidi ya kinidhamu.

Wakili wake tayari ameandikia klabu barua rasmi, akisisitiza uwezekano wa ukiukwaji wa kanuni za FIFA hususan kuhusu taratibu za kinidhamu na haki za wafanyakazi wa benchi la ufundi.


Historia ya Ramovic barani Afrika

Ramovic si mgeni katika soka la Afrika. Kabla ya kujiunga na CR Belouizdad mwaka 2025, aliwahi kuinoa TS Galaxy ya Afrika Kusini na Young Africans Sports Club (Yanga) ya Tanzania, ambapo alijijengea sifa kubwa.


Hatua zinazofuata

Ramovic anatarajiwa kufikishwa mbele ya kamati ya nidhamu siku ya Jumanne, ambapo uamuzi wa mwisho kuhusu mustakabali wake utaamuliwa. Hali hii inabaki kuwa kitendawili, huku mashabiki na waandishi wa habari wakisubiri kuona kama kocha huyo ataendelea kuinoa klabu hiyo au ataachishwa kazi.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.