Soka la Italia limeingia katika kipindi kigumu baada ya viongozi wakuu wa timu ya taifa kujiuzulu kufuatia kushindwa kufuzu kwa Kombe la Dunia, tukio lililozua mjadala mkubwa nchini humo na kimataifa.
Rais wa Shirikisho la Soka Italia (FIGC), Gabriele Gravina, ametangaza rasmi kuachia ngazi akichukua dhamana ya matokeo mabaya ya timu ya taifa. Hatua hiyo imekuja kufuatia presha kubwa kutoka kwa wadau wa michezo na viongozi wa kisiasa waliotaka mageuzi ya haraka ndani ya soka la nchi hiyo.
Sambamba na uamuzi huo, Mkuu wa Msafara wa timu ya taifa, Gianluigi Buffon, naye ametangaza kujiuzulu, akieleza kuwa ni hatua ya kuwajibika kwa kushindwa kwa timu hiyo kufikia malengo yake ya kufuzu.
Katika upande wa benchi la ufundi, kocha mkuu Gennaro Gattuso nae ameachia wadhifa wake kufuatia matokeo hayo mabaya.
Italia, mabingwa wa dunia mara nne, imeendelea kukumbwa na anguko la kiwango katika miaka ya karibuni, na kushindwa kufuzu kwa Kombe la Dunia mara ya pili mfululizo kumezidisha hali hiyo. Kushindwa huko kumeibua hasira kutoka kwa mashabiki na wachambuzi wa soka, waliotaka mabadiliko ya kina katika mfumo wa maendeleo ya soka nchini humo.
Shirikisho la soka la Italia linatarajiwa kuitisha mkutano maalum wa dharura kujadili mustakabali wa timu ya taifa, ikiwa ni pamoja na uteuzi wa uongozi mpya na maboresho ya kiufundi yatakayolenga kurejesha hadhi ya Italia katika soka la kimataifa.