Ligi Kuu ya NBC inaendelea leo amapo mechi tatu zinatarajiwa kupigwa katika viwanja mbalimbali.
Mabingwa watetezi wa ligi hiyo Yanga watakuwa dimba la nyumbani KMC Complex kuikabili Tanzania Prisons katika mchezo ambao utapigwa saa 12:30 jioni.
Baada ya kukosa ushindi katika mechi tatu zilizopita, ni wazi Wananchi leo 'wataikamia' Tanzania Prisons ambayo hata hivyo licha ya kuyumba msimu huu, kwenye mechi zilizopita wameonyesha wanaweza kupambana.
Yanga itaingia kwenye mchezo huo ikiwa imepata 'ahueni' baadhi ya nyota wake waliokuwa majeruhi wakirejea baada ya kupona.
Washambuliaji Prince Dube na Laurindo Aurelio 'Depu' wote walishiriki mazoezi ya mwisho ya Wananchi kuelekea mchezo huo na pengine huenda wakarejea kikosini leo sambamba na walinzi Ibrahim Hamad na Chadrack Boka.
Mechi ya mapema saa 10 itakuwa kule Kigoma dimba la Lake Tanganyika wakati wenyeji Mashujaa Fc watakapomenyana na Pamba Jiji katika mchezo mwingine unaotarajiwa kuwa na upinzani mkali.
Pamba Jiji wamekuwa na msimu bora mpaka sasa wakipania kumaliza nafasi nne za juu kwenye msimamo huku Mashujaa Fc nao wakijipanga upya chini ya kocha Jamhuri Kiwhelo 'Julio' baada ya kuyumba mwanzoni mwa msimu.
Namungo Fc wataikaribisha JKT Tanzania katika mchezo mwingine wa kukata na shoka ambao utapigwa uwanja wa Majaliwa saa 3 usiku.
