Klabu ya Barcelona imeendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa La Liga baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Atletico Madrid katika mchezo mkali uliopigwa jijini Madrid.
Ushindi huo muhimu umeongeza matumaini ya Barcelona kutwaa ubingwa msimu huu, hasa baada ya mpinzani wao mkubwa, Real Madrid, kupoteza mchezo wao mapema siku hiyo.
Katika pambano hilo, Atletico Madrid walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Giuliano Simeone dakika za mwishoni mwa kipindi cha kwanza. Hata hivyo, Barcelona walijibu haraka kupitia kwa Marcus Rashford aliyesawazisha dakika chache kabla ya mapumziko.
Mchezo huo ulibadilika kwa kiasi kikubwa baada ya Atletico kubaki na wachezaji 10 kufuatia Nico González kupewa kadi nyekundu mwishoni mwa kipindi cha kwanza, jambo lililoipa Barcelona nafasi ya kutawala mchezo katika kipindi cha pili.
Licha ya upinzani mkali kutoka kwa Atletico, mshambuliaji nyota Robert Lewandowski aliifungia Barcelona bao la ushindi katika dakika za mwisho, akimalizia mpira uliorudi kutoka kwa kipa.
Matokeo hayo yanaifanya Barcelona kujitanua kileleni kwa tofauti ya pointi saba dhidi ya Real Madrid baada ya kufikisha alama 76, huku zikiwa zimebaki takribani mechi nane kumaliza msimu.
Mapema, Real Madrid walipata pigo baada ya kufungwa 2-1 na Mallorca, matokeo ambayo yamevuruga kwa kiasi kikubwa hesabu zao za kuwania ubingwa na kuipa Barcelona nafasi kubwa zaidi ya kunyakuwa taji la La Liga msimu huu.



