Klabu ya Simba SC imekamilisha mchakato wa kumsajili kiungo mshambuliaji chipukizi kutoka Coastal Union, Bakari Msimu, katika hatua ya kuimarisha kikosi chake kuelekea msimu ujao.
Taarifa zinaeleza kuwa usajili wa mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 18 umependekezwa moja kwa moja na kocha mkuu wa Simba, Steven Barker, ambaye amevutiwa na kasi na uwezo wa ubunifu wa kiungo huyo mshambuliaji.
Simba imeingia makubaliano ya mkataba wa miaka mitatu na mchezaji huyo, hatua inayoashiria imani kubwa ya klabu kwa kipaji chake na mipango ya kumkuza kwa muda mrefu ndani ya kikosi hicho cha Wekundu wa Msimbazi.
Msimu amekuwa mmoja wa wachezaji wanaofanya vizuri katika kikosi cha Coastal Union msimu huu, akijipatia umaarufu kutokana na uwezo wake wa kucheza kasi na ubunifu mkubwa.
Msimu anakuwa mchezaji wa nne wa ndani kusajiliwa na Simba mapema katika maandalizi ya kikosi kipya, akiwa ameungana na Nathaniel Chilambo, Ramadhan Chobwedo na Kelvin Nashon.
Uongozi wa Simba umeweka mkakati wa kukamilisha usajili mapema kabla ya dirisha rasmi kufunguliwa, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kujiandaa mapema na msimu wa mashindano 2026/27.