Leo Juni 15, mikiki mikiki ya Kombe la Dunia 2026 inaendelea Mexico, Canada na marekani ambapo mechi kadhaa kali zinatarajiwa kuchezwa.
Moja ya mechi zinazovuta hisia za mashabiki wengi wa soka Afrika ni ile ya Spain dhidi ya Cape Verde, ambapo mabingwa wa Ulaya wanatarajiwa kuanza kampeni yao dhidi ya timu ya Cape Verde inayoshiriki Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza kabisa katika historia yake.
Huu ni mtihani mkubwa kwa Cape Verde, lakini pia ni nafasi ya kuonyesha kuwa hawakufika kimakosa. Mchezo huo utapigwa saa 1 usiku.
Kwa upande mwingine, macho ya Afrika pia yatakuwa kwenye pambano kati ya Belgium na Egypt saa 4 usiku, ambapo Misri inakutana na moja ya timu zenye wachezaji wenye uzoefu mkubwa wa ligi za Ulaya.
Misri inahitaji matokeo mazuri ili kujiweka katika mazingira bora ya kusonga mbele kwenye kundi gumu lenye ushindani mkubwa.
Mechi nyingine kubwa ni Saudi Arabia dhidi ya Uruguay, pambano linaloleta ladha ya Amerika Kusini dhidi ya Asia, huku Uruguay wakitazamiwa kutumia uzoefu wao wa mashindano ya kimataifa kukabiliana na kasi na nidhamu ya Saudi Arabia.
Pia kuna mchezo kati ya Iran na New Zealand, ambao unatarajiwa kuwa wa ushindani wa nguvu na mbinu, kila timu ikisaka pointi muhimu katika hatua za awali za makundi.



