Herve Renard kuinoa Tunisia katika mechi zilizobaki kombe la Dunia

Joel JJ By Joel JJ • 16th June 2026


Herve Renard kuinoa Tunisia katika mechi zilizobaki kombe la Dunia

Shirikisho la Soka la Tunisia limemteua kocha raia wa Ufaransa, Hervé Renard, kuwa kocha mkuu mpya wa timu ya taifa ya nchi hiyo kwa mechi zilizobaki za Kombe la Dunia 2026, kufuatia kufutwa kazi kwa Sabri Lamouchi baada ya kipigo kizito cha mabao 5-1 kutoka kwa Sweden kwenye mchezo wa kwanza wa Kundi F.

Kwa mujibu wa taarifa, Renard anatarajiwa kuwasili kambini kesho kukamilisha taratibu za kusaini mkataba kabla ya kuanza rasmi majukumu yake ya kuiongoza Tunisia katika mechi mbili zilizosalia hatua ya makundi dhidi ya Japan na Netherlands.

Lamouchi, ambaye aliteuliwa Januari mwaka huu kwa mkataba uliokuwa ukitarajiwa kudumu hadi 2028, amekuwa kocha wa kwanza kuondolewa kwenye Kombe la Dunia la 2026 baada ya matokeo mabaya dhidi ya Sweden. Uongozi wa soka wa Tunisia umeamua kufanya mabadiliko ya haraka ili kujaribu kufufua matumaini ya timu hiyo ya kusonga mbele kwenye mashindano.

Renard ni mmoja wa makocha wenye heshima kubwa barani Afrika. Ameandika historia kwa kutwaa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) akiwa na Zambia mwaka 2012 na Ivory Coast mwaka 2015, huku pia akijulikana kwa kuiongoza Saudi Arabia kuifunga Argentina katika moja ya matokeo ya kushangaza zaidi kwenye Kombe la Dunia la 2022.

Vyanzo vya karibu na Shirikisho la Soka la Tunisia vinaeleza kuwa uteuzi wa Renard haujalenga tu mechi zilizosalia za Kombe la Dunia, bali pia ni sehemu ya mpango wa muda mrefu wa kujenga kikosi kipya na kuimarisha ushindani wa timu hiyo katika miaka ijayo.

Tunisia kwa sasa ipo katika wakati mgumu baada ya kuanza kampeni yake kwa kipigo kikubwa dhidi ya Sweden. Hata hivyo, ujio wa Renard unaonekana kurejesha matumaini kwa mashabiki wa timu hiyo, wakiamini uzoefu wake mkubwa katika soka la kimataifa unaweza kuisaidia timu hiyo kufanya vizuri katika mechi zilizosalia dhidi ya Japan na Netherlands.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.