Azam FC imeendelea kuonyesha ubora wake katika Ligi Kuu ya NBC baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mashujaa FC katika mchezo uliochezwa leo dimba la Azam Complex.
Mabao ya Sadio Kanoute pamoja na James Akaminko yalitosha kuwapa Wanalambalamba pointi tatu muhimu mbele ya Mashujaa FC. Ushindi huo umeifanya Azam FC kuendelea kuimarisha nafasi yake ya tatu kwenye msimamo wa ligi baada ya kufikisha alama 58.
Azam FC ilionyesha dhamira ya kutafuta ushindi tangu dakika za mwanzo za mchezo, ikitawala sehemu kubwa ya mchezo na kuunda nafasi kadhaa za kufunga. Juhudi zao zilizaa matunda kupitia kwa Sadio Kanoute aliyefungua pazia la mabao kabla ya James Akaminko kuongeza bao la pili na kuhitimisha matumaini ya Mashujaa FC kurejea mchezoni.
Kwa ushindi huo, Azam FC inaendelea kuweka presha kwa timu zilizo juu yake kwenye msimamo wa ligi huku ikiongeza matumaini ya kumaliza msimu katika nafasi nzuri.
Kwa upande wa Mashujaa FC, matokeo haya yanaendelea kuongeza wasiwasi ndani ya kikosi hicho baada ya kupoteza mchezo wa pili mfululizo kwa idadi hiyo hiyo ya mabao. Katika mchezo wao uliopita, walifungwa mabao 2-0 na Yanga, hali inayoashiria kuwa timu hiyo inapitia kipindi kigumu katika hatua muhimu ya msimu.
Ni wazi kuwa vijana wa kocha Jamhuri Kihwelo wanapaswa kuamka haraka katika mechi zilizobaki ili kujinusuru na presha ya kushushwa hadi eneo la play-off, na pengine hatari ya kushuka daraja endapo matokeo hayatabadilika. Mashujaa FC wanahitaji kurejea kwenye kiwango chao haraka iwezekanavyo ili kuhakikisha wanabaki salama ndani ya Ligi Kuu ya NBC msimu huu.



