Klabu ya Azam FC imethibitisha rasmi kumuongezea mkataba kiungo wake mkongwe, Hemed Mao Mkami, ambaye ataendelea kubaki katika kikosi hicho hadi mwaka 2027.
Nyota huyo amesaini mkataba mpya wa mwaka mmoja ambao unaongeza muda wake wa kuitumikia klabu hiyo ya Chamazi, hatua inayoonesha imani kubwa ya benchi la ufundi na uongozi wa Azam FC kwa mchango wake ndani ya timu.
Himed Mao alirejea Azam FC msimu uliopita baada ya takribani misimu sita ya kucheza soka la kulipwa nchini Misri, ambako alijipatia uzoefu mkubwa katika mazingira ya ushindani wa juu. Uzoefu huo umeendelea kumfanya kuwa miongoni mwa wachezaji muhimu zaidi katika safu ya kiungo ya Azam FC.
Tangu kurejea kwake, Mao amekuwa na mchango mkubwa katika ujenzi wa timu, akicheza nafasi ya kiungo wa kati kwa nidhamu, uimara na uwezo wa kuongoza mchezo. Uwepo wake umeongeza uthabiti katika eneo la kiungo.
Hatua ya klabu hiyo kuongeza mkataba wa Himed Mao inaonesha dhamira ya Azam FC ya kubaki na msingi imara wa wachezaji wenye uzoefu, huku ikiendelea kujenga kikosi chenye mchanganyiko wa vijana na wazoefu.



