Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Pacome Zouzoua, ameweka wazi kuwa amekumbana na changamoto kubwa ya majeraha msimu huu, hali iliyomlazimu kucheza baadhi ya mechi akiwa na maumivu makali ya goti.
Nyota huyo, anayejulikana kwa uwezo wake mkubwa wa kutengeneza na kufunga mabao, amesema kipindi hicho kilikuwa kigumu kwake, lakini sasa ameimarika na yuko tayari kuisaidia Yanga katika mechi zilizosalia kabla ya kufungwa kwa msimu.
Pacome alionyesha kurejea katika kiwango chake bora baada ya kufunga bao la kwanza la Yanga kwenye ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Fountain Gate. Bao hilo lilikuwa muhimu kwake binafsi na kwa timu katika harakati za kutimiza malengo ya msimu.

Baada ya kufunga, Pacome alionyesha ishara maalumu ya shukrani kuelekea kwa mashabiki wa Yanga, akieleza kuwa ilikuwa ni njia yake ya kuwashukuru kwa sapoti waliompa katika kipindi chote alichokuwa akipambana na majeraha.
βIshara ile ni kuwashukuru mashabiki wa Yanga ambao wameweza kunivumilia katika kipindi kigumu. Nilicheza nikiwa na maumivu kwenye goti kwa kipindi kirefu kidogo lakini mara zote wamekuwa pamoja na mimi hata ninapokuwa katika nyakati ngumu uwanjani,β alisema Pacome.
Aliongeza kuwa bao alilofunga dhidi ya Fountain Gate lina maana kubwa kwake katika hatua hii muhimu ya mwisho wa msimu.
βGoli dhidi ya Fountain Gate ni muhimu sana kwangu katika wakati huu tunapoelekea mwisho wa msimu. Najiskia vizuri sasa na niko tayari kuwapa mashabiki wetu kile wanachokitarajia kutoka kwetu. Waje kwa wingi uwanjani kutusapoti kwenye mechi hizi za mwisho,β aliongeza.



