Licha ya kukosa sehemu kubwa ya msimu kutokana na majeraha, kiwango bora alichokionyesha golikipa Moussa Camara kabla ya kuumia kinaendelea kuwa kipimo kwa makipa wa Simba SC, hususan Djibrilla Kassali ambaye amebeba jukumu la kulinda lango la timu hiyo kwa kipindi kirefu cha msimu.
Akizungumza kuelekea fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB Bank pamoja na mwisho wa msimu wa Ligi Kuu ya NBC, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba SC, Ahmed Ally, amesema ubora aliouonesha Camara uliacha alama kubwa ndani ya kikosi hicho.
Ahmed Ally alieleza kuwa mashabiki na wadau wengi wa soka wamekuwa wakilinganisha kiwango cha makipa wa sasa na kile alichokionesha Camara kabla ya kuumia, jambo linaloonesha namna alivyokuwa muhimu ndani ya timu.
"Camara aliweka kiwango kikubwa sana kabla ya kuumia, ndiyo maana hata sasa watu bado wanakitaja na kukilinganisha na makipa waliopo. Hilo linaonesha ubora wake na mchango wake kwa timu," alisema Ahmed Ally.
Kwa sasa Simba inaendelea kujiandaa na michezo muhimu ya mwisho wa msimu huku ikitarajia kumaliza kampeni zake kwa mafanikio katika mashindano ya ndani.



