Makocha Yanga, Azam FC watambiana kuelekea nusu fainali Kombe la CRDB

Joel JJ By Joel JJ • 20th June 2026


Makocha Yanga, Azam FC watambiana kuelekea nusu fainali Kombe la CRDB

Makocha wa Yanga na Azam FC wameonyesha kujiamini huku wakitambiana kuelekea mchezo wa nusu fainali ya Kombe la CRDB unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.

Kocha wa Yanga, Abdihamid Moalin, amesema ni heshima kubwa kwa klabu hiyo kufanikiwa kucheza hatua ya nusu fainali ya mashindano hayo, huku akisisitiza kuwa lengo lao kuu ni kushinda mchezo huo na kutinga fainali.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari kuelekea mchezo huo, Moalin aliwapongeza wachezaji wake kwa kuendelea kuonyesha kiu ya mafanikio na ushindani wa hali ya juu katika mashindano mbalimbali.

“Tumewasili salama na maandalizi ya mchezo wa kesho yanaendelea vizuri. Wachezaji wako katika hali nzuri kiakili na kimwili na tunafahamu kile kinachohitajika kufanyika,” alisema Moalin.

Aliongeza kuwa uzoefu wa kikosi chake katika mechi kubwa ni moja ya silaha muhimu itakayowasaidia katika pambano hilo.

“Ni heshima kubwa kucheza nusu fainali ya mashindano kama haya. Tumestahili kufika hapa lakini lengo letu ni kufika fainali. Ili kufanya hivyo, tunapaswa kuwa bora katika wakati huu na kushinda kesho,” alisema.

Moalin pia aliwataka wachezaji wake kuendelea kuwa wanyenyekevu na wenye njaa ya ushindi licha ya mafanikio waliyoyapata katika misimu iliyopita.

“Tunapaswa kubaki wanyenyekevu, wenye njaa ya mafanikio na tusichoke kushinda. Kushinda ni jambo la kipekee ambalo timu nyingi zinatamani kulifikia. Huu ni mwaka mwingine na fursa nyingine ya kuandika historia mpya,” alisisitiza.

Aidha, aliwaomba mashabiki wa Yanga kujitokeza kwa wingi kuisapoti timu yao katika mchezo huo muhimu.

Kwa upande wa Azam FC, Kocha Mkuu Florent Ibenge amesema anatambua ugumu wa kukabiliana na Yanga, lakini amesisitiza kuwa kikosi chake kimejiandaa vya kutosha kuhakikisha kinapata ushindi na kufuzu hatua ya fainali.

“Tunajua ni mchezo mgumu dhidi ya Yanga lakini sisi tumejiandaa kimbinu kuweza kushinda. Tumecheza nao mara tatu, mechi moja tumetoka sare na tumepoteza mechi mbili, moja ikiwa kwa mikwaju ya penalti. Matokeo haya yanaonyesha hatuko mbali nao,” alisema Ibenge.

Kocha huyo raia wa DR Congo aliongeza kuwa licha ya Yanga kuonekana kuwa na nafasi kubwa kutokana na ubora wao wa hivi karibuni, Azam FC itaingia uwanjani ikiwa na lengo moja tu la kuibuka na ushindi.

“Najua wao watakuwa juu kwenye mchezo huo lakini sisi tutakuwa tayari na tunataka kushinda ili tuweze kufuzu fainali,” alisema.

Mchezo huo wa nusu fainali ya Kombe la CRDB utapigwa kesho Jumapili Juni 21 katika uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.


  

More Stories

Makocha Yanga, Azam FC watambiana kuelekea nusu fainali Kombe la CRDB
Makocha Yanga, Azam FC watambiana kuelekea nusu fainali Kombe la CRDB
Today, READ MORE →
Nyota Paraguay amekula umeme kwa kuziba mdomo
Nyota Paraguay amekula umeme kwa kuziba mdomo
Today, READ MORE →
Kivuli cha Camara kinavyomtesa Kassali Simba
Kivuli cha Camara kinavyomtesa Kassali Simba
Today, READ MORE →
Brazil yatinga kileleni kundi C baada ya kuichapa Haiti 3-0
Brazil yatinga kileleni kundi C baada ya kuichapa Haiti 3-0
Today, READ MORE →
Morocco yaizamisha Scotland, yabeba matumaini ya Afrika
Morocco yaizamisha Scotland, yabeba matumaini ya Afrika
Today, READ MORE →
Mutale na Simba wafikia makubaliano ya kuvunja mkataba
Mutale na Simba wafikia makubaliano ya kuvunja mkataba
Today, READ MORE →
Pacome afunguka changamoto ya majeraha, atoa ahadi kwa Wananchi
Pacome afunguka changamoto ya majeraha, atoa ahadi kwa Wananchi
Today, READ MORE →
Himid aongeza mwaka Azam Fc
Himid aongeza mwaka Azam Fc
Yesterday, READ MORE →
Kone kuuguza majeraha kwa miezi 6
Kone kuuguza majeraha kwa miezi 6
Yesterday, READ MORE →
Makocha Simba, Coastal Union wafunguka maandalizi nusu fainali CRDB Cup
Makocha Simba, Coastal Union wafunguka maandalizi nusu fainali CRDB Cup
Yesterday, READ MORE →