Klabu ya Real Madrid imetoa taarifa rasmi ikikanusha ripoti zilizosambaa katika vyombo mbalimbali vya habari zikidai kuwa imefikia makubaliano ya masharti binafsi na winga wa Bayern Munich, Michael Olisé.
Kupitia taarifa hiyo, mabingwa hao wa kihistoria barani Ulaya wamesema hawajawahi kufanya mawasiliano yoyote, ya moja kwa moja wala yasiyo ya moja kwa moja, na mchezaji huyo au mawakala wake kuhusu uwezekano wa uhamisho.
“Kwa kujibu taarifa zilizochapishwa na vyombo mbalimbali vya habari kuhusu madai ya kuvutiwa na mchezaji wa Bayern Munich, Michael Olisé, Real Madrid inapenda kuweka wazi kwamba haijafanya mawasiliano yoyote ya moja kwa moja au yasiyo ya moja kwa moja na mchezaji huyo wala mawakala wake,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Real Madrid pia ilisisitiza kuwa ina uhusiano mzuri wa muda mrefu na Bayern Munich, ukijengwa juu ya heshima, ushirikiano na kuaminiana kati ya klabu hizo mbili kubwa barani Ulaya.
Klabu hiyo imeeleza kuwa taarifa za kuwepo kwa makubaliano kati yake na Olisé si za kweli, huku ikibainisha kuwa taratibu za heshima za taasisi zinahitaji mazungumzo yoyote kuhusu mchezaji wa klabu nyingine kuanza kwanza kati ya klabu husika.
“Klabu zote mbili zimekuwa zikidumisha uhusiano unaotokana na kuaminiana na kuheshimiana. Hali hiyo inaakisi imani ya pamoja kwamba masuala yoyote yanayohusu mchezaji wa klabu moja yanapaswa kujadiliwa kwanza kati ya taasisi hizo mbili kwa kuzingatia misingi ya uaminifu wa kitaasisi,” iliongeza taarifa hiyo.
Tamko hilo linaonekana kuzima uvumi uliokuwa ukienea kuhusu mustakabali wa Olisé, ambaye amekuwa akihusishwa na vilabu kadhaa vikubwa vya Ulaya kutokana na kiwango chake bora cha uchezaji.



