Klabu ya Manchester City imefikia makubaliano ya kumsajili kiungo wa kati Elliot Anderson kutoka Nottingham Forest kwa pauni milioni 130, hatua inayoripotiwa kuvunja rekodi mpya ya uhamisho wa wachezaji nchini Uingereza.
Ripoti zinaeleza kuwa Anderson mwenye umri wa miaka 23 ameiomba rasmi Nottingham Forest kumpa ruhusa ya kujiunga na Manchester City, huku akionyesha nia ya wazi ya kuhamia Etihad Stadium. Uchunguzi wake wa kimatibabu unatarajiwa kufanyika katika siku zijazo, ikiwa ni sehemu ya kukamilisha uhamisho huo mkubwa.
Awali, Nottingham Forest walikataa ofa mbili kutoka Manchester City kabla ya kufikia makubaliano ya mwisho ya kifurushi chenye thamani ya takribani Β£130 milioni ikijumuisha bonasi. Klabu hiyo inatarajiwa kupata faida kubwa ya zaidi ya Β£80 milioni kutokana na uwekezaji wao wa awali kwa mchezaji huyo.
Anderson anatajwa kuwa sehemu muhimu ya mipango ya kikosi cha Manchester City kutokana na uwezo wake wa kucheza nafasi mbalimbali katikati ya uwanja, akichanganya uchezaji wa kiufundi, ulinzi na uwezo wa kuanzisha mashambulizi kwa pasi za mbali na ubunifu mkubwa.
Kwa upande wa City, usajili huu unaonekana kama mwanzo wa mradi mpya wa kuimarisha kikosi chao kuelekea misimu ijayo, huku Elliot Anderson akitarajiwa kuwa moja ya vipande muhimu katika mfumo mpya wa kiufundi wa klabu hiyo



