Timu ya taifa ya Ivory Coast imeandika ukurasa mpya katika historia yake baada ya kufuzu hatua ya 32 bora ya Kombe la Dunia 2026 kwa mara ya kwanza, kufuatia ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Curaçao katika mchezo wa mwisho wa Kundi E uliopigwa Philadelphia Stadium.
Ushindi huo uliiwezesha Ivory Coast kumaliza nafasi ya pili katika kundi hilo kwa pointi sita nyuma ya Ujerumani, na hivyo kuvunja mwiko wa muda mrefu wa kushindwa kuvuka hatua ya makundi katika michuano ya Kombe la Dunia walizoshiriki awali.
Katika mchezo huo wa kihistoria, mshambuliaji Nicolas Pépé alikuwa nyota wa usiku baada ya kufunga mabao mawili, likiwemo bao la mapema dakika ya saba lililokuja kutokana na makosa ya ulinzi wa Curaçao. Mabao hayo yaliwapa Les Éléphants utulivu na kuudhibiti mchezo hadi kipenga cha mwisho.
Safari ya Ivory Coast katika Kundi E haikuwa nyepesi. Katika mchezo wa kwanza walishinda 1-0 dhidi ya Ecuador kupitia bao la dakika za mwisho lililofungwa na Amad Diallo, kabla ya kupoteza 2-1 dhidi ya Ujerumani katika mchezo ulioshuhudia mabao ya Franck Kessié na mshambuliaji wa Ujerumani Deniz Undav aliyeibadilisha matokeo.
Hata hivyo, ushindi dhidi ya Curaçao umekuwa muhimu zaidi katika historia ya taifa hilo, ukifuta maumivu ya miaka mingi ya kushindwa kuvuka makundi katika mashindano ya 2006, 2010 na 2014, licha ya kuwa na vikosi vilivyokuwa na majina makubwa na matarajio makubwa.
Kwa mara ya kwanza kabisa, Ivory Coast sasa wataonekana katika hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia, hatua ambayo imeleta furaha kubwa nchini humo na katika bara la Afrika kwa ujumla, ikizingatiwa kwamba timu hiyo imekuwa moja ya nguzo muhimu za soka la Afrika katika miaka ya hivi karibuni.
Ivory Coast sasa watakabiliwa na mshindi wa Kundi I katika hatua ya 32 bora itakayochezwa Julai 3, 2026, wakiwa na matumaini ya kuendeleza mafanikio yao mapya na kuandika sura nyingine ya kihistoria katika safari yao ya Kombe la Dunia 2026.



