Kocha Mkuu wa Simba SC, Steve Barker, amesema kikosi chake kinatarajia mchezo wa ushindani dhidi ya Singida BS utakaochezwa kesho, akisisitiza kuwa lengo kuu ni kutumia nafasi zitakazopatikana na kuondoka na alama tatu. Akizungumza na waandishi wa habari kabla ya mchezo huo, Backer amesema anaiheshimu Singida BS na anaamini haitakuwa mechi rahisi.
Barker amesema maandalizi ya timu yamekamilika na wachezaji wanaelewa umuhimu wa mchezo huo katika mbio za ubingwa wa NBC Premier League. Ameeleza kuwa katika hatua hii ya msimu, makosa madogo yanaweza kugharimu timu, hivyo amewataka wachezaji wake kucheza kwa umakini tangu dakika ya kwanza hadi ya mwisho.
Kwa upande wake, mchezaji wa Simba, Anthony Mligo, amesema mechi kati ya Simba na Singida BS mara zote huwa na ushindani mkubwa, lakini akaongeza kuwa kikosi hicho kimejiandaa vya kutosha kukabiliana na changamoto hiyo. Mligo alisema lengo lao ni kupata ushindi ili kuendelea kujiweka katika nafasi nzuri kwenye mbio za ubingwa.
Singida BS nao wanaingia kwenye mchezo huo wakisaka matokeo mazuri dhidi ya Simba. Timu hiyo imeonyesha ushindani katika baadhi ya mechi za msimu huu, jambo linaloifanya Simba kutolichukulia kirahisi pambano hilo licha ya kucheza mbele ya mashabiki wao.
Mchezo huo unakuja wakati ushindani wa kileleni mwa msimamo wa ligi ukiwa mkali, huku Simba ikihitaji ushindi ili kuendelea kuisukuma mbio za ubingwa. Kupoteza alama katika hatua hii ya msimu kunaweza kuathiri malengo ya timu, hivyo kila mchezo uliobaki una umuhimu mkubwa.
Mashabiki wa Simba wanatarajia kuona timu yao ikirejea kwenye kiwango bora na kupata ushindi muhimu dhidi ya Singida BS. Kauli za Backer na Mligo zimeonyesha dhamira ya kikosi hicho, lakini matokeo halisi yataamuliwa ndani ya dakika 90 uwanjani wakati timu hizo zitakapokutana.



