Pamba Jiji FC inaweza kuingia kwenye kipindi kigumu cha kujenga upya kikosi baada ya kumalizika kwa msimu wa NBC Premier League, huku taarifa zikieleza kuwa idadi ya wachezaji wake huenda ikaondoka kuelekea msimu ujao.
Hali hiyo inatajwa kuchangiwa na changamoto mbalimbali za ndani ya klabu pamoja na kuvutiwa kwa baadhi ya nyota wake na timu nyingine zinazotafuta kujiimarisha. Kwa mujibu wa taarifa zinazozungumzwa ndani ya duru za soka, baadhi ya wachezaji wa Pamba Jiji tayari wanatajwa kuwa kwenye mazungumzo na klabu tofauti kwa ajili ya uhamisho wa msimu ujao.
Wapo wanaomaliza mikataba yao, huku wengine wakitajwa kutafuta changamoto mpya baada ya msimu kumalizika. Mbali na hilo, kumekuwa na madai ya kuwepo kwa sintofahamu ndani ya kikosi, ikiwemo baadhi ya wachezaji wazawa kudai kutopata nafasi ya kutosha, jambo linalodaiwa kuathiri morali ndani ya timu.
Aidha, zipo tetesi zinazoeleza kuwa baadhi ya wachezaji walionesha kutoridhishwa na hali inayoendelea klabuni, ingawa hakuna taarifa rasmi iliyotolewa kuthibitisha madai hayo. Miongoni mwa majina yanayotajwa kuhusishwa na tetesi hizo ni Matthew Teges Momanyi na Kelvin Nashon, huku ikisubiriwa kuona kama Pamba Jiji itafanikiwa kuwabakisha nyota wake muhimu au itaanza msimu mpya ikiwa na sura mpya kabisa ya kikosi.



