Kumeibuka taharuki kuelekea mchezo muhimu wa hatua ya 32 bora ya Kombe la Dunia 2026 kati ya Mexico na Ecuador, baada ya mamia ya mashabiki wa Mexico kukusanyika nje ya hoteli inayofikia timu ya taifa ya Ecuador wakipiga honi za magari, tarumbeta, spika na kuimba nyimbo usiku kucha.
Taarifa zinaeleza kuwa baadhi ya wachezaji wa Ecuador walionekana wakichungulia madirishani kuona kilichokuwa kikiendelea, huku mashabiki hao wakidaiwa kupanga kuendelea na kelele hizo usiku mzima kwa lengo la kuwanyima wapinzani wao usingizi kabla ya mchezo huo muhimu.
Hatua hiyo imezua mjadala mkubwa miongoni mwa mashabiki wa soka duniani, ambapo baadhi wanaiona kama mbinu ya kuwapa Mexico faida ya nyumbani, huku wengine wakisema inakiuka misingi ya mchezo wa haki (fair play) na heshima kwa wapinzani.
Mexico na Ecuador zinakutana saa 4:00 usiku (EAT) wa kuamkia kesho mjini Mexico City, katika pambano ambalo mshindi atafuzu hatua ya 16 bora ya Kombe la Dunia 2026. Macho ya dunia sasa yataelekezwa uwanjani kuona kama kelele hizo zitakuwa na athari yoyote kwa maandalizi ya Ecuador au kama watajibu kwa matokeo ndani ya dakika 90.



