Yanga SC imeendelea kuandika historia katika soka la Tanzania baada ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC kwa msimu wa tano mfululizo, rekodi inayodhihirisha ubora na uthabiti wa klabu hiyo katika ushindani wa ligi.
Wananchi walihakikisha ubingwa huo kufuatia ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya JKT Tanzania katika mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa Isamuhyo. Ushindi huo umeifanya Yanga kufikisha mataji 32 ya Ligi Kuu katika historia ya klabu hiyo.
Mshambuliaji Prince Dube aliifungia Yanga bao la kwanza mapema kabisa katika dakika ya 9, bao lililowapa utulivu na kuwawezesha kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa bao 1-0.
Hata hivyo, kabla ya kipindi cha kwanza kumalizika, mashabiki wa Yanga walipatwa na simanzi baada ya kiungo mshambuliaji Pacome Zouzoua kupata majeraha mabaya kufuatia tukio lililomhusisha beki wa JKT Tanzania, Twalib Hassan. Baada ya tukio hilo, mwamuzi alimpa Twalib kadi nyekundu.
Kipindi cha pili, Yanga iliendelea kutawala mchezo na kuthibitisha ubora wake kwa kuongeza mabao mawili zaidi kupitia Maxi Nzengeli na Laurindo Aurelio "Depu", na kuhitimisha mchezo kwa ushindi mnono wa mabao 3-0.
Licha ya kupitia kipindi chenye changamoto na misukosuko katika msimu huu, Yanga imeonyesha uimara, mshikamano na ari ya kupambana hadi mwisho, jambo lililowezesha kutimiza lengo lao kubwa la kutwaa ubingwa kwa mara nyingine.
Watani zao Simba wameibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya KMC hata hivyo matokeo hayo hayajatosha kuwapa ubingwa kwani wamefikisha alama 73 huku Wananchi wakisepa na ubingwa wakiwa na alama 75.
Wakati Yanga ikibeba ubingwa, Mtibwa Sugar inaungana rasmi na KMC kushuka daraja baada ya kupigwa mabao 2-2 dhidi ya Namungo Fc.
Tanzania Prisons na Mbeya City zinatarajiwa kucheza mechi za play-off kuwania kusalia ligi kuu.Β



