Klabu ya Tottenham Hotspur imeendelea kuonyesha nguvu kubwa katika soko la uhamisho baada ya kufikia makubaliano ya rekodi ya klabu ya pauni milioni 100 kumsajili kiungo wa Newcastle United, Sandro Tonali, huku pia ikikamilisha dili jingine kubwa la Mateus Fernandes kutoka West Ham.
Kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa na Sky Sports, Tottenham wamekubaliana kulipa jumla ya pauni milioni 100 kwa Tonali, ikiwa ni pamoja na Β£92.5 milioni ada ya awali na Β£7.5 milioni nyongeza zinazoweza kufikiwa.
Kiungo huyo wa kimataifa wa Italia mwenye umri wa miaka 26 anatarajiwa kusafiri kutoka Milan kuelekea London siku ya Alhamisi kwa ajili ya vipimo vya afya na kukamilisha taratibu za uhamisho wake. Pia inaripotiwa kuwa Tonali atakuwa akilipwa zaidi ya Β£275,000 kwa wiki, hatua inayoonyesha dhamira kubwa ya Spurs kumfanya mmoja wa wachezaji wanaolipwa zaidi klabuni hapo.
Ripoti zinaeleza kuwa Tonali alivutiwa na mradi wa kocha wa Spurs, Roberto De Zerbi, raia mwenzake wa Italia, licha ya kuwaniwa pia na klabu nyingine kubwa kama Manchester City.
Katika hatua nyingine, Spurs wamekubaliana pia dau la rekodi ya klabu la pauni milioni 85 kumsajili kiungo chipukizi wa West Ham, Mateus Fernandes, katika dili la pili kubwa mfululizo ndani ya siku mbili.
Usajili wa Tonali na Fernandes unatarajiwa kuifanya Tottenham kuvuka kiwango cha matumizi ya zaidi ya pauni milioni 200 katika dirisha hili la usajili, ishara ya wazi ya mabadiliko makubwa ya kisera ndani ya klabu hiyo.
Mbali na wachezaji hao wawili, Spurs pia wameshatumia pauni milioni 52 kumsajili beki Jan Paul van Hecke kutoka Brighton. Pia wameongeza uzoefu kikosini kwa kusajili Andy Robertson, Marcos Senesi na Martin Dubravka kwa uhamisho wa bure.



