Shirikisho la Soka la Ujerumani (DFB) linatarajiwa kuanza zama mpya baada ya taarifa kwamba kocha Julian Nagelsmann ameondoka kwenye nafasi ya ukocha mkuu kufuatia kampeni mbaya ya Ujerumani kwenye Kombe la Dunia 2026.
Nagelsmann amefikia mwisho wa safari yake baada ya Ujerumani kutolewa mapema na Paraguay katika hatua ya 32 bora, matokeo yaliyoongeza presha kubwa kwa uongozi wa DFB.
Ingawa shirikisho bado halijatoa tamko rasmi kuhusu mrithi wake, JΓΌrgen Klopp ameibuka kuwa mgombea anayepewa nafasi kubwa zaidi kuchukua usukani wa timu hiyo.
Klopp, ambaye kwa sasa anafanya kazi ndani ya mfumo wa Red Bull kama Mkuu wa Soka Duniani, ameripotiwa kuwa tayari kusikiliza pendekezo kutoka DFB ikiwa mazungumzo yataanza rasmi. Ripoti zinaeleza kuwa mazingira ya mkataba wake yanaweza kuruhusu kuondoka endapo ataitwa kuiongoza timu ya taifa ya Ujerumani.
Kocha huyo mwenye umri wa miaka 59 amekuwa akitajwa mara kadhaa kama chaguo la muda mrefu la kuinoa Ujerumani kutokana na mafanikio yake makubwa akiwa Borussia Dortmund na Liverpool, ambako alishinda Ligi Kuu England, UEFA Champions League pamoja na mataji mengine makubwa.
Hata hivyo, hadi sasa hakuna makubaliano rasmi yaliyotangazwa kati ya Klopp na DFB. Taarifa zilizopo zinaonyesha kuwa mazungumzo yanatarajiwa kufanyika katika siku zijazo huku DFB ikitaka kumpata kocha atakayerejesha hadhi ya taifa hilo baada ya kushindwa kufanya vizuri katika Kombe la Dunia mara tatu mfululizo.
Iwapo Klopp atakubali jukumu hilo, ataanza kazi kubwa ya kujenga upya kikosi cha Die Mannschaft na kurejesha ushindani wa moja ya mataifa yenye historia kubwa zaidi katika soka la dunia.



