Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba SC, Crescentius Magori, amesema klabu hiyo imerejea kwenye njia ya ubingwa baada ya kutwaa taji la CRDB Federation Cup leo, akieleza kuwa mafanikio hayo ni ishara ya maendeleo ambayo timu imeyapata msimu huu.
Akizungumza mara baada ya ushindi huo, Magori amesema Simba imefanikiwa kufikia moja ya malengo yake kwa kutwaa kombe hilo, huku akisisitiza kuwa kikosi hicho kimeonyesha uwezo mkubwa katika mashindano yote kilichoshiriki msimu huu.
"Simba imerejea kwenye njia ya ubingwa, tumebeba kombe hili la CRDB, lakini kama ligi ingekuwa ya haki, msimu huu tungebeba makombe yote mawili," alisema Magori.
Kauli hiyo imeibua mjadala miongoni mwa wadau wa soka nchini kutokana na madai yake kuhusu mwenendo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, huku ikija wakati Simba ikihitimisha msimu kwa kutwaa taji la CRDB Federation Cup na kuongeza idadi ya makombe yake katika historia ya mashindano hayo.



