Kiungo na nahodha wa Newcastle United, Bruno Guimarães, ameripotiwa kuufahamisha uongozi wa klabu hiyo kuwa anataka kuondoka mwishoni mwa msimu na kujiunga na mabingwa wa Ligi Kuu England, Arsenal. Taarifa hizo zikieleza kuwa Arsenal wameongeza juhudi za kumfuatilia nyota huyo wa Brazil.
Arsenal wanadaiwa kuwa tayari kuwasilisha ofa ya pauni milioni 60 kwa ajili ya kumsajili Guimarães, baada ya ofa yao ya awali ya pauni milioni 55 kukataliwa na Newcastle. Hata hivyo, hadi sasa hakuna mazungumzo rasmi yaliyoanza kati ya klabu hizo mbili, huku Newcastle wakiendelea kumthamini mchezaji huyo kwa zaidi ya pauni milioni 100.
Licha ya msimamo wa Newcastle kutokuwa tayari kumuuza nahodha wao, taarifa zinaeleza kuwa nia ya Guimarães ya kutafuta changamoto mpya inaweza kubadili mwelekeo wa mazungumzo. Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 28 bado ana mkataba unaomalizika mwaka 2028, lakini kukosekana kwa nafasi ya kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya kunatajwa kuwa sababu kubwa ya kutaka kuondoka.
Iwapo uhamisho huo utakamilika, Newcastle watapoteza mmoja wa wachezaji wao muhimu na nahodha aliyekuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya klabu hiyo, huku Arsenal wakitarajia kuongeza nguvu kwenye safu yao ya kiungo kuelekea msimu mpya.