Beki wa Arsenal na Timu ya Taifa ya Ufaransa, William Saliba, anakabiliwa na uwezekano wa kufanyiwa upasuaji baada ya kupata jeraha la mgongo katika mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Dunia dhidi ya Hispania, mchezo ambao Ufaransa ilipoteza kwa mabao 2-0, huku Saliba akitolewa uwanjani mapema kutokana na maumivu aliyoyapata.
Ripoti kutoka gazeti la Ufaransa, L’Équipe, zinaeleza kuwa upasuaji unaweza kuwa suluhisho linalowezekana kutokana na tatizo hilo ambalo tayari lilikuwa limemsumbua kwa kipindi fulani.
Endapo vipimo vitathibitisha ulazima wa kufanyiwa upasuaji, Arsenal wanatarajiwa kukaa bila huduma ya beki huyo kwa kipindi cha miezi minne hadi mitano. Hilo litakuwa pigo kubwa kwa klabu hiyo kuelekea mwanzo wa msimu mpya wa Ligi Kuu England, kutokana na nafasi muhimu ambayo Saliba amekuwa nayo katika kikosi cha Mikel Arteta.
Saliba alikuwa miongoni mwa wachezaji muhimu wa Arsenal msimu uliopita, akicheza mechi 50 katika mashindano mbalimbali, ikiwemo dakika zote 120 za fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Paris Saint-Germain. Kukosekana kwake kutamlazimisha Arteta kutafuta suluhisho jipya la safu ya ulinzi, huku Cristhian Mosquera akitajwa kuwa mmoja wa wachezaji wanaoweza kupewa nafasi ya kushirikiana na Gabriel Magalhães.