Simba SC imepokea bonasi ya Shilingi milioni 78,765,000 kutoka kwa mdhamini wao mkuu, Betway Tanzania, ikiwa ni tuzo maalum kwa mafanikio ya klabu hiyo ya kutwaa Kombe la CRDB Federation Cup msimu wa 2025/26. Bonasi hiyo inaongezwa juu ya zawadi ya ushindi ya Tsh milioni 125 waliyoipokea kutoka kwa wadhamini wa kombe hilo, CRDB Bank.
Ushindi huo ulipatikana baada ya Simba kuwafunga Azam FC kwa bao 1-0 katika fainali iliyochezwa Julai 4, 2026 katika Uwanja wa Gombani, Pemba, Zanzibar. Bao pekee la mchezo huo lilifungwa dakika ya 62 kupitia bao la kujifunga la kiungo wa Azam Yahya Zayd, aliyeingiza mpira mlangoni mwao wenyewe, hatua iliyowapa Simba ushindi wa mwisho baada ya mchezo mgumu na wenye ushindani mkubwa.
Taji hilo lilimaliza kiu ya miaka minne ya Simba ya kukosa ubingwa mkubwa wa ndani, na pia lilikamilisha "double" ya makombe ya ndani chini ya kocha Steve Barker, ambaye awali aliwaongoza kutwaa Kombe la Muungano mapema mwaka huu. Ushindi huo pia uliwaongezea Simba mfululizo wa mechi 30 bila kushindwa katika mashindano yote.
Kwa sasa Simba wanaendelea na maandalizi ya msimu mpya wa 2026/27 chini ya Barker, wakiwa tayari wamehakikisha nafasi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF Champions League) msimu ujao, baada ya kumaliza nafasi ya pili katika Ligi Kuu NBC nyuma ya mabingwa Young Africans.