Klabu ya Yanga SC imeendelea kufanya maboresho makubwa kwenye kikosi chake kwa lengo la kuendelea kutawala soka la Tanzania baada ya misimu mitano mfululizo ya mafanikio.
Miongoni mwa maeneo ambayo mabingwa hao wameonekana kulipa kipaumbele ni nafasi ya kiungo mkabaji, ambapo taarifa zinaeleza kuwa mchakato wa kumnasa nyota wa Nigeria, Morrice Chukwu, umefikia hatua za mwisho.
Chukwu kwa sasa ni mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na Singida Black Stars. Klabu hiyo kutoka mkoani Singida ilikuwa kwenye mipango ya kumuongezea mkataba mpya, lakini mazungumzo hayo yanadaiwa kuvurugika baada ya Yanga kuingia kwenye mbio za kuwania saini yake.
Ikiwa mambo yataenda kama yanavyopangwa, Chukwu anatarajiwa kujiunga na Yanga SC na kuimarisha safu ya kiungo ya timu hiyo. Hatua hiyo inakuja wakati Singida BS ikimpokea tena Mohamed Damaro ambaye amerejea baada ya kumalizika kwa muda wake wa mkopo wa miezi sita.
Chukwu amekuwa mmoja wa wachezaji muhimu kwenye kikosi cha Singida BS kwa misimu miwili iliyopita, akionyesha uwezo mkubwa katika nafasi ya kiungo mkabaji pamoja na kucheza kama beki wa kati pale inapohitajika.