Klabu ya Simba SC imeendelea kuimarisha kikosi chake kwa ajili ya msimu mpya baada ya kumtambulisha rasmi kiungo mahiri raia wa Nigeria, Ibraheem Jabaar, ambaye ametua Msimbazi kama mchezaji huru akitokea Stellenbosch FC ya Afrika Kusini.
Jabaar mwenye umri wa miaka 23 amejiunga na Simba baada ya kumalizika kwa mkataba wake na Stellenbosch, ambapo aliamua kutouhuisha licha ya juhudi za klabu hiyo kumshawishi kubaki.
Ripoti zinaeleza kuwa ushawishi wa aliyekuwa kocha wake, Steve Barker, ambaye aliwahi kufanya kazi naye kwa mafanikio makubwa Stellenbosch, ulikuwa miongoni mwa sababu zilizorahisisha hatua ya nyota huyo kujiunga na wekundu hao wa Msimbazi.
Katika kipindi chake akiwa Stellenbosch, Jabaar alionyesha kiwango bora kilichomfanya kuwa mmoja wa viungo muhimu wa timu hiyo. Aidha, aliwahi kupata uzoefu wa kucheza kwa mkopo katika klabu ya Maccabi Petah Tikva ya Israel, hatua iliyompa nafasi ya kuongeza makali na uzoefu wa kimataifa.
Moja ya sifa kubwa za Jabaar ni uwezo wake wa kucheza nafasi mbalimbali. Mbali na kucheza kama kiungo wa kati, anaweza pia kutumika kama kiungo mshambuliaji pamoja na winga wa kushoto, jambo linalompa kocha wa Simba chaguo zaidi katika kupanga kikosi.
Usajili wa Jabaar unatarajiwa kuongeza ubora katika safu ya kiungo ya Simba huku mashabiki wakiamini atakuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya timu hiyo katika mashindano ya ndani na kimataifa msimu ujao.