Serikali imesema Tamasha la Taifa litakuwa nyenzo muhimu katika kulinda, kutunza na kuendeleza utamaduni wa Mtanzania, huku likitumika pia kuimarisha utaifa na mshikamano, kukuza uchumi bunifu, kufungua fursa za ajira na biashara, pamoja na kuitangaza Tanzania kupitia utalii wa kiutamaduni.
Akitoa taarifa kuhusu maandalizi ya tamasha hilo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amesema tamasha hilo linatarajiwa kufanyika mkoani Morogoro kuanzia Agosti 25 hadi 29, 2026.
Msigwa amesema tamasha hilo litawakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya utamaduni na ubunifu, likiwemo vikundi 28 vya utamaduni, wasanii 30, wajasiriamali 70 pamoja na vijana 5,000.
Amesema uwepo wa makundi hayo unalenga kutoa nafasi kwa washiriki kuonyesha vipaji, bidhaa na kazi zao za ubunifu, huku wananchi wakipata fursa ya kujifunza na kufurahia utajiri wa tamaduni mbalimbali zinazopatikana nchini.
Kwa mujibu wa Msigwa, tamasha hilo pia ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha utamaduni wa Tanzania unatambulika zaidi ndani na nje ya nchi, sambamba na kutumia utamaduni kama chanzo cha fursa za kiuchumi, ajira na biashara kwa wananchi, hasa vijana.
Aidha, ametoa rai kwa wananchi kushiriki kwa wingi katika Tamasha la Taifa ili kupata nafasi ya kushuhudia na kujifunza mambo mbalimbali yanayohusiana na utamaduni wa Mtanzania, ikiwemo ngoma za asili, vyakula vya asili na mavazi ya asili.
Mbali na burudani na maonesho ya kitamaduni, tamasha hilo pia litakuwa na mdahalo wa kitaifa utakaojikita katika kuwawezesha vijana kushiriki katika kulinda maadili, hatua ambayo Serikali inaamini itasaidia kujenga kizazi kinachothamini utamaduni na misingi ya maadili ya taifa.
Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa utamaduni katika kujenga umoja wa kitaifa na kukuza uchumi, huku Tamasha la Taifa likitarajiwa kuwa moja ya majukwaa yatakayounganisha utamaduni, ubunifu, biashara na utalii kwa manufaa ya Watanzania.



