Simba SC imeandaa mpango maalum wa kusafiri na mashabiki wake kwenda Malawi wakati timu hiyo ikianza kampeni za Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF Champions League) msimu wa 2026/27.
Simba itaanza safari yake ya kimataifa kwa kukutana na Mighty Wanderers ya Malawi katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa hatua ya awali, unaotarajiwa kuchezwa Septemba 6, 2026, nchini Malawi.
Mchezo wa marudiano umepangwa kufanyika Septemba 13, 2026, jijini Dar es Salaam, huku Simba ikitarajiwa kutangaza uwanja utakaotumika baadaye.
Simba kusafiri na mashabiki Malawi
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, amesema klabu hiyo imeandaa basi maalum litakalowapeleka mashabiki Malawi ili kuipa timu sapoti ya kutosha katika mchezo huo muhimu wa kimataifa.
Kwa mujibu wa Ahmed, safari ya mashabiki itaanza Septemba 3, 2026, saa 1:00 usiku kutoka Dar es Salaam kuelekea Lilongwe, Malawi. Mashabiki watakusanyika Ubungo katika kituo cha Engen kabla ya kuanza safari.
Simba inalenga kuwa na angalau mabasi matatu kwa ajili ya mashabiki, huku safari hiyo ikielezwa kuwa ya kifahari na yenye lengo la kuwapa mashabiki nafasi ya kuisindikiza timu yao katika hatua hii ya michuano.
“Kwa kuwa tunakwenda Malawi, tumeandaa safari ya basi la mashabiki kwenda Malawi. Tumeshawahi kusafiri huko nyuma kwa basi kwenda Malawi, Zambia na hata Uganda. Safari hii tunakwenda kucheza na Mighty Wanderers tukasema tusiiache timu iende peke yake,” alisema Ahmed Ally.
Akaongeza: “Safari hii tunarejea tena Malawi na safari hii tunataka kuvunja rekodi ya kusafiri na mashabiki wengi.”
Passport ni sharti kwa mashabiki
Mashabiki wanaopanga kusafiri wameelekezwa kuwa na hati halali ya kusafiria. Ahmed Ally amesema sharti hilo litazingatiwa ili kuepusha usumbufu wakati wa safari.
“Kama unataka kwenda Malawi sharti la kwanza uwe na hati ya kusafiria (passport). Kama huna basi anza hata mchakato wa kutafuta ile ya karatasi, Malawi wanaruhusu pia ile ya karatasi. Kuepusha usumbufu, hatapanda mtu ambaye hana passport,” alisema.
Mashabiki wanaotaka kuweka nafasi ya safari hiyo wametakiwa kupiga simu kupitia namba 0742-771311 kwa ajili ya oda na kupata maelezo zaidi kuhusu safari.
Simba kuanza safari ya CAFCL kwa hamasa
Safari hiyo ya mashabiki inakuja wakati Simba ikijiandaa kurejea katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika ikiwa na malengo makubwa ya kufanya vizuri zaidi msimu huu.
Ahmed Ally amesema klabu imefanya tathmini ya msimu uliopita na kuchukua hatua mbalimbali, ikiwemo kusajili wachezaji wenye uzoefu mkubwa, ili kuimarisha kikosi kwa ajili ya mashindano ya kimataifa.
“Ya mwaka jana yalishapita, tulifanya uchambuzi wa kutosha, tumesajili wachezaji wakubwa na wenye uzoefu mkubwa. Ni imani yetu mwaka huu tutavuka hatua ya makundi na kwenda robo fainali,” alisema Ahmed.
Simba imeweka wazi kuwa haitaki kuishia katika hatua za awali au makundi pekee, bali inalenga kufika mbali zaidi katika mashindano hayo. Kwa mujibu wa Ahmed, lengo kubwa la klabu msimu huu ni kufika hatua ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Hivyo, mchezo dhidi ya Mighty Wanderers utakuwa mwanzo wa safari hiyo, huku Simba ikitarajia kupata matokeo mazuri nchini Malawi kabla ya mchezo wa marudiano Septemba 13, 2026, Dar es Salaam.



