Kiungo wa kimataifa wa Tanzania, Alphonce Mabula Msanga, hatimaye ameibukia katika klabu ya JS Kabylie ya Algeria, baada ya kuhusishwa kwa nguvu na mabingwa wa Tanzania, Yanga SC, katika dirisha lililopita la usajili.
Mabula, mwenye umri wa miaka 23, amejiunga na JS Kabylie kama mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na klabu ya Shamaxi FK ya Azerbaijan mwishoni mwa Juni 2026.
Taarifa kutoka Algeria zinaeleza kuwa amesaini mkataba wa miaka mitatu na klabu hiyo ya Tizi Ouzou.
Usajili huo ulikamilika katika siku ya mwisho ya dirisha la usajili nchini Algeria, huku JS Kabylie ikifanikiwa kuipita klabu nyingine zilizokuwa zikimuwania kiungo huyo.
Yanga ilimtaka Mabula
Kabla ya kuibukia Algeria, jina la Mabula lilikuwa gumzo kwenye dirisha la usajili nchini Tanzania baada ya Yanga kuanza mazungumzo ya kumrudisha nyumbani.
Iliripotiwa mwezi Julai kwamba Yanga ilikuwa imeanza mazungumzo na Mabula, ikiwa na lengo la kumuongeza katika eneo la kiungo mkabaji. Wakati huo Mabula alikuwa amemaliza mkataba wake na Shamaxi na alikuwa mchezaji huru.
Baadaye, taarifa zikaeleza kuwa mazungumzo hayo hayakuzaa matunda kutokana na tofauti za kifedha ambapo upande wa Mabula ulihitaji ofa ya uhamisho iliyokadiriwa kufikia karibu Sh1.5 bilioni, pamoja na mshahara wa takribani dola 14,000 kwa mwezi, huku Yanga ikiishia kwenye ofa ya zaidi ya Sh600 milioni ambayo haikukidhi mahitaji ya upande wa mchezaji.
Kabla ya dili la Yanga kufifia, pia Mabula alikuwa akihusishwa na Kasimpasa ya Uturuki, huku taarifa za awali zikidai klabu hiyo ilikuwa ikimfuatilia kwa karibu.



