Kiungo mshambuliaji wa Simba SC, Clatous Chama, ameweka wazi kipindi kigumu alichopitia baada ya kuondoka Msimbazi na kujiunga na watani wao wa jadi, Yanga SC, akisema uamuzi huo ulimletea majuto makubwa.
Chama amesema siku aliyosaini mkataba na Yanga haikuwa siku nzuri kwake, akieleza kuwa alijutia uamuzi huo na baadaye alijaribu kuwasiliana na uongozi wa Yanga ili kurejesha kila kitu na kurejea Simba, lakini ombi lake lilikataliwa. “Nilimpigia Rais wa Yanga na kumwambia narudisha kila kitu ili nirudi Simba, lakini akakataa,” amesema Chama.
Akizungumzia zaidi kipindi hicho, Chama amesema hakuwahi kupanga kujiunga na Yanga na kwamba uamuzi huo ulitokea bila kuwa sehemu ya mipango yake. Hata hivyo, amesema kurejea Simba kulimletea furaha yeye pamoja na familia yake, huku kwa sasa akiendelea kuitumikia klabu hiyo na kuchangia katika msimu huu.



