Klabu ya TRA United inatajwa kumteua kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Tanzania, Hemed Suleiman (56), kuwa kocha mpya wa timu hiyo, akichukua nafasi ya Etienne Ndayiragije ambaye alitimuliwa siku chache zilizopita.
Hemed anarejea kwenye soka la ushindani akiwa na jukumu la kuiongoza TRA United katika kipindi ambacho timu hiyo inatafuta mwendelezo mzuri wa matokeo.
Ujio wa Hemed unafuatia taarifa za awali zilizohusisha TRA United na kocha wa zamani wa Mbeya City, Meckie Mexime, ambaye inadaiwa alisimamia mazoezi ya timu hiyo siku ya Jumanne wakati klabu ikiwa katika mchakato wa kumpata kocha mpya.
Hata hivyo, TRA United imeamua kumpa nafasi Hemed, ambaye ana uzoefu mkubwa katika soka la Tanzania, ikiwemo kipindi alichokuwa sehemu ya benchi la ufundi la Taifa Stars.
Kocha huyo sasa anakabiliwa na jukumu la kuijenga upya TRA United na kuhakikisha timu hiyo inapata matokeo yatakayoiweka kwenye nafasi nzuri baada ya kuanza kwa kuchechea katika msimu huu.