Kocha wa Yanga SC, Manqoba Mngqithi, amesema bado hajafikia uamuzi wa mwisho kuhusu kikosi kitakachoanza katika mchezo dhidi ya Geita Gold, kutokana na muda mfupi wa maandalizi na kutokuwa na picha kamili ya hali ya baadhi ya wachezaji waliopata majeraha katika mchezo uliopita.
Mngqithi amesema, “Kwa hatua hii ni vigumu kusema kama kutakuwa na mabadiliko gani kwenye timu kuelekea mchezo wetu wa kesho. Bado hatujafanya mazoezi kamili na hatujajua kwa uhakika hali ya majeruhi na wachezaji waliopata majeraha madogo kwenye mchezo uliopita. Hata hivyo, ni wazi kutakuwa na baadhi ya mabadiliko.”
Kocha huyo pia amesema hana presha licha ya ushindani mkubwa uliopo katika ligi, akieleza kuwa yupo katika nafasi ambayo amekuwa akiitamani. Mngqithi amesisitiza umuhimu wa kuchukua kila mchezo kwa wakati wake, huku akitambua kuwa Yanga bado haijakutana na baadhi ya timu kubwa kwenye ligi.
“Sina presha, niko kwenye nafasi ambayo nilitamani kuwa. Tunapaswa kufurahia ushindani na kuona mapambano yataishia wapi. Hii ni ligi yenye ushindani mkubwa na bado hatujacheza dhidi ya baadhi ya timu kubwa, hivyo tunapaswa kuchukua mchezo mmoja baada ya mwingine,” amesema Mngqithi.
Mngqithi ameongeza kuwa bado kuna maeneo mengi ambayo Yanga inahitaji kuyaboresha, lakini changamoto kubwa ni ukosefu wa muda wa kutosha wa mazoezi kutokana na ratiba ya mashindano. Kocha huyo anaamini mapumziko ya FIFA yanaweza kuwapa nafasi ya kufanya maboresho zaidi, ikiwemo kuongeza utimamu wa baadhi ya wachezaji.
Akizungumzia mashabiki wa Yanga, Mngqithi amewashukuru kwa namna ambavyo wameendelea kuwa pamoja na timu katika ratiba yao ngumu. Amesema sapoti yao imekuwa muhimu na amewaomba waendelee na utamaduni huo wa kuisapoti timu katika kila mchezo.
“Tunawahitaji kesho waje kwa wingi na watupatie nguvu kama mchezaji wetu wa 12, ili kwa pamoja tuhakikishe tunapata ushindi,” amesema Mngqithi.
Yanga SC itashuka dimbani kesho saa 1:00 usiku kuikabili Geita Gold, huku Mngqithi akitarajia kupata ushindi mbele ya Wananchi na kuendelea kujenga mwendelezo mzuri wa timu katika NBC Premier League.