Maandalizi ya klabu ya Yanga kuelekea mchezo wao wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) dhidi ya Gaborone United ya Botswana, yameshika kasi huku homa ya pambano hilo ikipanda Wananchi wakiendelea kununua tiketi kwa wingi.
Mchezo huo unaotarajiwa kupigwa keshokutwa Jumamosi, Septemba 12, 2026, kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku Yanga ikipania kuandikish ushindi muhimu nyumbani mbele ya mashabiki wake ili kufuzu raundi ya kwanza ya michuano hiyo.
Wapinzani wa Yanga, Gaborone United, wanatarajiwa kuwasili nchini leo Alhamisi wakitokea jiji kuu la Gaborone, Botswana tayari kwa mchezo huo wa mkondo wa pili baada ya sare ya bao 1-1 kwenye mchezo wa kwanza.
Sare hiyo iliwapa Yanga mtaji wa bao la ugenini, lililofungwa na mshambuliaji Selemani Mwalimu 'Gomez' ambaye mechi ya Jumamosi itatumika kumuheshimisha mbele ya Wananchi.
Meneja wa Habari wa Yanga, Ally Kamwe amewasihi mashabiki kuendelea kununua tiketi za VIP B (Tsh 10,000) na Mzunguko (Tsh 5,000) baada ya tiketi za VIP A kumalizika.
Aidha kutokana na uwanja wa Azam Complex kuchukua mashabiki wachache, uongozi wa Yanga umepanga kuweka skrini kubwa ('Big Screen') nje ya uwanja wa Chamazi ili kila shabiki ashuhudie burudani hiyo.