Mshambuliaji wa Yanga Seleman Mwalimu 'Gomez' amewaalika mashabiki wa timu hiyo kujitokeza kwa winga uwanja wa Azam Complex hapo kesho katika mchezo wa mkondo wa pili hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika (CAFCL) dhidi ya Gaborone United.
Akizungumza katika mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Mwalimu alisema ni heshima kubwa kwake kuwa sehemu ya wachezaji wanaokwenda kuipambania nembo ya Yanga katika mchezo huo.
Amesema wachezaji wote wako tayari na wanaichukulia mechi hii kwa uzito mkubwa kwa sababu imebeba hatma yao ya kufuzu raundi ya kwanza ya ligi ya mabingwa.
Licha ya kutambua ugumu wa mchezo huo, Mwalimu amesema wamekuwa na wakati mzuri wa maandalizi kwenye uwanja wa mazoezi akiamini kwenye uwezo wa benchi la ufundi chini ya kocha Manqoba Mngqithi katika kuwasoma wapinzani na hivyo wataingia kwenye mchezo huo na mbinu sahihi zitakazowahakikishia ushindi.
“Tunaichukulia mechi hii kwa ukubwa wake, kwa sababu ni mechi yenye hatma yetu kimataifa msimu huu. Benchi letu la ufundi limefanya kazi kubwa kuhakikisha tunatengeneza mipango bora. Tumejipanga vizuri kuhakikish tunapata ushindi. Malengo yetu ni kuhakikisha tunafika mbali katika michuano hii ya Kimataifa.”
“Yanga kwa sasa tuna kocha mkubwa. Tayari ameona ubora na udhaifu wa mpinzani. Kwenye kiwanja cha mazoezi mwalimu na benchi lake la ufundi wametuelekeza namna ya kucheza na wapinzani wetu. Presha ambayo tumepeleka Botswana tutaipeleka hapa mara mbili. Nina matumaini kabla ya kipindi cha pili tutakuwa na matokeo sahihi”
“Nina washukuru viongozi na mashabiki kwa kuandaa mchezo huu kupitia jina langu. Ninafarijika sana kuona klabu inatambua mchango wangu. Kwangu hili ni deni kubwa ambalo napaswa kulipa. Timu ina wachezaji wengi lakini ukiona wameita mechi kwa jina lako basi ujue kuna heshimu kubwa sana unapata kutoka kwa hao watu. Niwahakikishie tutajitoa kwa zaidi ya asilimia 100,” alisema Mwalimu