Mabingwa wa Tanzania Bara, Yanga SC, leo wanakabiliwa na kibarua cha kuamua hatima yao katika Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), watakaposhuka Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, kuikabili Gaborone United ya Botswana katika mchezo wa mkondo wa pili wa hatua ya awali.
Mchezo huo unakuja wakati Yanga ikilenga kuendeleza rekodi yake nzuri katika raundi hatua za awali, baada ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 katika mchezo wa kwanza uliopigwa nchini Botswana.
Mtanange huo unaotarajiwa kuamua timu itakayofuzu kwenda raundi ya kwanza ya michuano hiyo, umepangwa kuanza saa 1:00 usiku.
Yanga imekuwa na historia nzuri katika hatua ya awali ya CAFCL kwa misimu minne iliyopita, ikiwa haijapoteza mchezo wowote wa raundi ya kwanza na mara nyingi imekuwa ikitawala wapinzani wake kwa ushindi mkubwa.
Msimu wa 2022/23, Yanga iliifunga Zalan FC mabao 4-0 ugenini na 5-0 nyumbani. Msimu uliofuata, 2023/24, ilishinda dhidi ya ASAS Djibouti 2-0 ugenini na 5-1 nyumbani.
Katika msimu wa 2024/25, Yanga iliendeleza ubabe kwa kuifunga Vital'O ya Burundi 4-0 ugenini na 6-0 katika mchezo wa marudiano, kabla ya msimu wa 2025/26 kuichapa Wiliete ya Angola 3-0 ugenini na 2-0 nyumbani.
Hata hivyo, msimu huu mambo yameanza tofauti baada ya Gaborone United kuizuia Yanga kupata ushindi katika mchezo wa kwanza, matokeo ambayo yameongeza umuhimu wa mchezo wa leo.
Kwa Yanga, ushindi wowote utaihakikishia tiketi ya kusonga mbele, huku sare ya 0-0 pia ikiwa na matokeo ya kuipa nafasi kutokana na kanuni ya mabao ya ugenini.
Macho ya mashabiki wa Yanga sasa yanaelekezwa Chamazi, ambako timu yao itatafuta ushindi na kuendeleza safari yake ya kuwania taji la Afrika.